Tanzania
This article was added by the user . TheWorldNews is not responsible for the content of the platform.

BRELA yaita wadau AGRF kufanya usajili majina ya biashara, kampuni zao

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni nchini (BRELA) umetoa wito kwa wafanyabiashara na wadau mbalimbali walioshiriki katika Mkutano wa Mifumo ya Chakula Afrika (AGRF 2023) kufika katika banda lao ili kuweza kupata huduma wanazozitoa ikiwemo kufanya usajili wa majina ya biashara na kampuni zao.

Hayo yamebainishwa leo na Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano BRELA, Roida Andusamile wakati akizungumza na waandishi wa habari katika mkutano huo wa AGRF 2023 unaoendelea jijini Dar es Salaam kwenye Ukumbi wa Mikutano ya Kimataifa wa Mwalimu Nyerere (JNICC).

Amesema BRELA inawaomba washiriki wa mkutano huo wa AGRF 2023 kufika katika banda lao lililopo chini ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) ili kupata usaidizi wa usajili ya majina ya biashara, kampuni, alama za biashara na huduma pamoja na utoaji wa leseni za biashara kundi A na za viwanda.

“Kama mnavyojua masuala yote ya usajili Brela tunafanya kwa njia ya mtandao, sisi tumeshatoka analogia na tupo digitali zaidi, hivyo huduma zetu zote tunazitoa kwa njia ya digitali na kama kuna changamoto yoyote kwenye mfumo tunamuhudumia mteja papo kwa papo,” amesema na kuongeza

“Kwa muda huu uliyobakia tunawakaribisha sana wadau wetu wafike katika banda letu ili wapate huduma hizi za Brela kwa urahisi zaidi,” amesema

Aidha amesisitiza kuwa wanatambua kuwa washiriki wa mkutano huo wakiwemo wakulima ni wadau wao wakubwa na kwamba kilimo ni biashara hivyo Brela wanaingia kwa lengo la kuhakikisha mkulima anaweza kurasimisha biashara yake.

Written by Janeth Jovin